Saturday 15 March 2014

Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Kitaifa Yafikia Kilele Jijini Tanga Leo



Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Haki za Mlaji Kitaifa yamefikia kilele leo kwa maandamano ya wakazi wa Jiji la Tanga, burudani na hotuba zilizotolewa katika viwanja vya Tropikana Mabawa, Jijini Tanga.

Kilele cha maadhimisho hayo kilitanguliwa na maandamano ya wakazi wa jiji la Tanga walioongozwa na Bendi ya Muziki wa Ala (Brass Band) na kuwahusisha wanafunzi wa Shule za Sekondari za Mikanjuni, Popatlal na Usagara pamoja na Chuo Kikuu cha Eckenforde.

Maandamano hayo yaliyoanzia katika viwanja vya Uhuru Park majira ya saa nne asubuhi, yalipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Mhe. Halima Dendegu majira ya saa tano asubuhi. Mhe. Dendegu ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho hayo.

Akihutubia katika kilele cha maadhimisho hayo, Mhe. Dendegu alizitaka kampuni za simu kupitia na kurekebisha taratibu na kanuni zao za utendaji ili kuhakikisha kuwa wanazitambua na kuzilinda haki za watumiaji wa simu ili kuwezesha matumizi ya huduma ya mawasiliano ya simu kuwa ya tija. Alisema bils kuzingatia haki za watumiaji wa simu, ni vigumu kupatikana kwa matumizi yenye tija, jambo linaloweza kuathiri ukuaji endelevu wa sekta hiyo nchini. 

Aidha, Mhe. Dendegu aliwataka watumiaji wa simu kubadilisha miondoko na mienendo ya kutumia simu kwa lengo la kuwezesha matumizi mazuri kuzingatiwa ili matumizi hayo yaweze kuwa na tija.

Pamoja na kutoa rai kuhusu matumizi ya simu, Mhe. Dendegu pia aliwataka wananchi kuwa makini wanapokwenda kufanya manunuzi yao sokoni kwa kuhakikisha kuwa wanatimiza wajibu wao kwa kukagua na bidhaa wanazotaka kununua badala ya kuzikimbilia kutokana na urahisi wa bei.  

Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Haki za Mlaji kwa mwaka 2014 Kitaifa yamebebwa na Kaulimbiu isemayo “Haki za Watumiaji wa Simu Zilindwe”. Kauli mbiu hiyo inalenga kuzitaka Kampuni za Simu kubainisha Haki za Msingi za Watumiaji wa Huduma za Simu na kisha kuweka utaratibu wa kuzilinda haki hizo, hasa ikizingatiwa kuwa maendeleo ya Sayansi na Teknolojia pamoja na Utandawazi, vimesababisha matumizi ya simu hususan za mkononi kuwa makubwa sana ambapo inakadiriwa kuwa zaidi ya watu bilio tano ulimwenguni kote wanatumia huduma ya simu za mkononi.

No comments:

Post a Comment