Saturday 5 April 2014

Vyombo vya Udhibiti, Mahakama, Wafanyabiashara Timizeni Wajibu Wenu-Mulongo



Vyombo vya Udhibiti, Mahakama, Wafanyabiashara Timizeni Wajibu Wenu-Mulongo

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Magesa Mulongo amevitaka vyombo vya usimamizi wa uchumi na udhibiti wa biashara na huduma pamoja na wafanyabiashara kwa ujumla kutimiza wajibu wao ili kuhakikisha kuwa ukiukaji wowote wa sheria za nchi unaowaumiza walaji ambao ni wananchi wa Tanzania, hauachwi bila wahusika kuchukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa Sheria za nchi

Mhe. Mulongo alitoa wito huo wakati akifungua Semina ya siku moja kwa wadau wa Sheria ya Ushindani, Utetezi wa Mlaji na Udhibiti wa Bidhaa bandia, iliyoandaliwa na Tume ya Ushindani na kufanyika katika Hoteli ya Kibo Palace, jijini Arusha.

Mhe. Mulongo alisema kuwa kumekuwa na malalamiko mahali pengi kutokana na utendaji usioridhisha wa vyombo mbalimbali vya udhibiti na usimamizi wa utendaji wa mfumo wa uchumi wa soko na kuitaka Tume ya Ushindani kuusoma mfumo mzima wauzalishaji na usambazaji wa bidhaa bandia na kuchukua hatua kabla ya bidhaa hizo hazijaingizwa sokoni kwa kuwa mfumo huo utakapodhibitiwa vema, itakuwa vigumu kwa wafanyabishara wasio waaminifu kuweza kuuza bidhaa hizo sokoni.

Aidha alivitaka vyombo hivyo kufanya kazi kwa pamoja badala ya kila kimoja kufanya kazi kivyake kwa kuwa utendaji wa pamoja utawezesha kila chombo kutoa mchango wake stahiki katika kudhibiti mienendo potofu na kandamizi katika uchumi kwa kuwa wafanyabiahara wasio waaminifu watatambua mamlaka ya Serikali na vyombo vyake katika kusimamia na kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Alibainisha kuwa yamekuwepo malalamiko ya utendaji kwa baadhi ya vyombo vya udhibiti vya Serikali pamoja na mahakama, na kuwa mashauri yameonekana kutoshughulikiwa kwa weledi na hivyo kusababisha  wahalifu kuachiwa kwa sababu zinazowavunja moyo wananchi na kusababisha kutoviamini vyombo vya Serikali vinavyotoa haki katika kutimiza majukumu yao.

Mada mbalimbali ziliwasilishwa katika Semina hiyo ikiwa ni pamoja na Dhana na Maudhui ya Sheria ya Ushindani, Muundo wa Sheria ya Ushindani, Utetezi wa Mlaji na Mapambano Dhidi ya Bidhaa Bandia.

Wadau walijadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupendekeza kuifanyia marekebisho sheria ya alama za bidhaa ili wahalifu wanaojihusisha na biashara za bidhaa bandia zenye madhara kwa binadamu washitakiwe kwa “kusudio la kufanya mauaji”. Aidha, wajumbe wengine walielezea umuhimu wa elimu ya utetezi wa mlaji kusambazwa kuanzia ngazi za shule za msingi ili jamii ijayo ya Watanzania ikue ikiwa na uelewa mzuri zaidi wa masuala ya msingi ya haki na wajibu wa mlaji na kuwa tayari kutetea haki zake na kufhamu wajib wake awapo sokoni.

Aidha, Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) Mkoa, walitangaza azma ya kuratibu mchakato wa kuanzisha Chama cha Walaji Mkoani Arusha na kuwataka washiriki wa Semina kujitokeza kuwa wanachama waasisi wa chama hicho.
 
Semina hiyo ilihudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi wa Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, wawakliishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Idara ya Maliasili, Maafisa Biashara na Ushirika wa Mikoa, Wilaya na JIji, Wawaklishi wa Taasisi za Wafanyabiashara, Wafanyabiashara na wazalishaji na waandishi wa habari.

No comments:

Post a Comment