TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Prof. Mkenda Amtambulisha Kaimu
Mkurugenzi Mkuu Mpya, Dk. John Mduma Kwa Wafanyakazi wa FCC
Awataka
Wafanyakazi Kuendelea Kufanya Kazi Nzuri kwa Weledi na Uadilifu Zaidi
Dar
es Salaam, Agosti 29, 2017. Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na
Uwekezaji (Biashara), Prof. Adolph
Mkenda, amemtambulisha Kaimu Mkurugenzi Mkuu Mpya wa Tume ya Ushindani (FCC),
Dk. John Kedi Mduma, katika Mkutano Maalum na Menejimenti na wafanyakazi hao
uliofanyika mchana katika ukumbi wa Mikutano wa FCC, Jengo la GEPF House,
Agosti, 28, 2017.
Akizungumza katika kikao cha utambulisho huo, Prof.
Mkenda alisema kuwa anafahamu kuwa kazi ya Tume ni ngumu na muhimu sana kwa
uchumi wa taifa na hivyo akawataka wafanyakazi kuendelea kufanya kazi nzuri
wanayoifanya kwa weledi na kwa uadilifu zaidi ili kutunza heshima ya Serikali
na Taasisi na kuhakikisha kuwa azma ya Serikali ya Kuwa na Uchumi wa Viwanda
inafanikiwa.
Alisema kuwa Serikali haitakubali kuona kuwa
wafanyabiashara wasio waaminifu wanaingiza na kuuza bidhaa bandia bila
kuchukuliwa hatua stahiki kwa kuwa bidhaa hizo ambazo mara nyingi huwa chini ya
kiwango na huuzwa kwa bei chee, husababisha wazalishaji wa bidhaa halisi na
zinazokidhi viwango kusita kufungua viwanda hapa nchini kwa kuwa hawataweza
kushindana na bidhaa bandia zinazoharibu sökö.
“Serikali ipo pamoja nanyi, tutawalinda na kuwatetea,
chapeni kazi, misogope na msikate tamaa na msimamie kwenye sheria. Isipokuwa
sasa mnatakiwa kufanya kazi zenu kwa uadilifu na weledi zaidi ili taswira nzuri
ya taasisi iendelee kulindwa”, alisisitiza Prof. Mkenda. Aliwataka wafanyakazi kumpa
ushirikiano mkubwa Kaimu Mkurugenzi MkuuDk. John Mduma, katika kuhakikisha kuwa
taasisi inapiga hatua zaidi katika kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa
sheria.
Prof. Mkenda aliwapongeza wafanyakazi wa FCC kwa kufanya
kazi nzuri kwa weledi na uadilifu katika mazingira magumu ya uhaba wa
rasilimali na vitendea kazi na kuelezea kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono
na kuboresha maslahi yao kadiri hali itakavyoruhusu.
“Madhali mnaongeza uchapaji kazi na maslahi yanakwenda
kuwa mazuri zaidi na madhali kazi yenu inakwenda kuwa muhimu kuliko wakati
wote, mtaangaliwa zaidi kuliko wakati wowote ili kubaini nani anakwamisha
juhudi za Serikali. Kwa hiyo wakati mnafanya kazi nzuri, asitokee mmoja kati
yenu atakayeharibu sifa yenu nzuri,” alisisitiza Prof. Mkenda.
“Serikali haitawaingilia katika maamuzi yenu ya
kimahakama bali patakapokuwa na maswali tutawauliza na msichoke kutujibu ili
tuweze kuelewa ukweli ulivyo. Kazi yenu ni ngumu na inasababisha mpigwe majungu
na kusingiziwa mambo mbali mbali, hivyo tunalazimika kuuliza. Muilinde taswira
ya taasisi yenu kwa kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na weledi kama mnavyolinda
mboni ya jicho,” aliasa Prof. Mkenda na kuongeza kuwa kamwe Serikali
haitavumilia kampuni zinazotaka kuimairisha ukiritimba (Monopoly) katika soko
kwa kuwa zinawakandamiza walaji wa bidhaa na huduma na kuua ushindani katika
soko na hivyo akawataka watendaji wa Tume kuendelea kuchukua hatua kwa mujibu
wa sheria lakini waepuke pia kutumia lugha za kibabe na kuwaasa wawasaidie
wafanyabiashara (hususan kuhus suala la kuingiza bidhaa bandia) kwa lugha
wezeshi ili wasitumbukie tena kwenye hatari ya kuagiza bidhaa bandia na
kukamatwa mara kwa mara.
Kabla ya kumtambulisha Dk. Mduma, Prof. Mkenda
alimpongeza Dk. Frederick Shadrack Ringo kwa kuiendesha Taasisi hiyo kwa weledi
kwa kipindi cha muhula wake wa miaka minne na kumtakia kila la kheri baada ya
kuhitimisha muhula wa uongozi wake FCC.
Aidha, Dk. Frederick Ringo aliezea shukrani zake kwa
imani ambayo Serikali ilimpa katika kuiongoza Tume ya Ushindani pamoja na
ushirikiano alioupata kutoka kwa wafanyakazi wa Tume na viongozi wa Serikali.
Alisema kutoka na na ushirikiano huo
FCC imeweza kupiga hatua zaidi kuliko alivyoikuta. Aidha, alimweleza
Katibu Mkuu kuwa kuwa kwa sasa taasisi ina upungufu wa wafanyakazi zaidi ya 50
na inahitaji kuwa na ofisi ya kudumu pamoja na ghala za kuhifadhi bidhaa bandia
zinazosubiri kukamilika kwa hatua za kisheria kabla ya kuteketezwa.
Akizungumza baada ya kutambulishwa kwa wafanyakazi,
Dk. John Mduma alielezea kufurahishwa kwake na mapokezi mazuri aliyoyapata lakini
akabainisha kuwa ataelezea viapumbele vyake wakati atakapozungumza na
wafanyakazi baada ya kukabidhiwa rasmi ofisi mapema hivi karibuni.
Dk. John Kedi Mduma, ambaye ni Mchumi na Mhadhiri wa
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ameteuliwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.
Charles Mwijage (MB) kushika wadhifa huo kuanzia tarehe 28 Agosti, 2017 baada
ya muhula wa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Dk. Frederick Shadrack
Ringo (Wakili) kuisha Agosti 1, 2017. Prof. Mkenda alisema kuwa Dr. Mduma
ameteuliwa kushika wadhifa huo kwa kipindi cha mpito wakati ambapo taratibu za
uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu mpya zikiendelea kukamilishwa kwa mujibu wa Sheria ya
Ushindani Na. 8 ya mwaka 2003.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasilaino na Mahusiano ya Umma, Tume ya Ushindani, Dar es
Salaam.
Kwa
Maelezo zaidi wasiliana na Frank S. Mdimi. Afisa Mwandamizi, Mawasiliano na
Mahusiano ya Umma, Tume ya Ushindani, Simu ya Mkononi +255784762437, Barua Pepe
fmdimi@competition.or.tz
No comments:
Post a Comment