Friday 19 September 2014

Notisi ya Tume ya Ushindani kwa Wafanyabiashara Nchini Tanzania


NOTISI YA TUME YA USHINDANI KWA WAFANYABIASHARA NCHINI TANZANIA

(Imetolewa chini ya Kifungu Na. 9(1)(b) cha Sheria ya Ushindani, 2003)

Sheria ya Ushindani, Namba 8 ya Mwaka 2003 imetungwa kwa ajili ya kulinda na kushajiisha ushindani wa dhati katika mfumo wa uchumi wa soko na kumlinda mlaji/mteja dhidi ya mbinu na mienendo potofu na onevu ya kibiashara.

Ili kusimamia kwa ufanisi misingi ya ushindani katika uchumi wa soko na kuhakikisha kuwa mlaji/mteja analindwa ipasavyo, Sheria hii imekataza mambo kadhaa ambayo yamegawanywa katika  mafungu makubwa matatu ambayo ni:

a) Makubaliano yanayokiuka ushindani (Anti-competitive agreements) (Vifungu vya 8 na 9).
b)   Matumizi mabaya ya nguvu ya soko (Misuse of Market Power) (kifungu cha 10).
c) Miungano ya Kampuni inayoimarisha hodhi ya soko (Mergers and Acquisitions, Kifungu cha 11).

Hivi karibuni, ilisikika katika vyombo vya habari kuwa wafanyabiashara sehemu mbalimbali nchini, bila ya kuwajali walaji/wateja wao,  waliamua kufanya mgomo na kufunga biashara zao kwa sababu ya kulalamikia utumiaji wa mashine za kielektroniki za kutoa risiti kwa mteja (EFD), jambo lisilowahusu wateja wao. Mgomo huo ulileta  usumbufu na kuwaumiza zaidi walaji/wateja kwani hawakuweza kupata bidhaa na huduma walizohitaji kwa wakati na wengine kupata hasara.

Kwa mujibu wa taarifa za habari, vitendo vya namna hii vya wafanyabiashara vinaendelea kushamiri siku hadi siku na wanasahau kuwa Sheria ya Ushindani inazuia vitendo kama hivyo.  Sheria ya Ushindani katika kipengele cha 9(1)(b) inazuia washindani katika biashara kuingia katika makubaliano ya kugoma kuuza bidhaa au huduma kwa sababu kitendo hicho husababisha mlaji (consumer)/mteja (customer) kukosa haki yake ya kisheria ya kupata bidhaa au huduma muhimu.

Kutokana na ufafanuzi huu hapo juu, Tume ya Ushindani inatoa notisi hii kwa wafanyabiashara wote nchini kuwa:-

1)   Kufanya mgomo wa kuuza bidhaa na huduma  kwa walaji/wateja ni kinyume cha Sheria ya Ushindani, Na. 8/ 2003, na hatua za kisheria zinaweza kuchukuliwa dhidi yao.

2)   Jitihada za kutanzua migogoro ya kibiashara kati yao na taasisi za Serikali haziwahusu walaji/wateja wao na kitendo chochote cha kuwaumiza walaji na kuzuia ushindani katika soko ni kinyume cha Sheria ya Ushindani, Na. 8/ 2003, na hatua za kisheria zinaweza kuchukuliwa dhidi yao.
POKEA NOTISI HII KUWA Tume ya Ushindani itafanya uchunguzi wa migomo iwapo itatokea tena kwa mjibu wa Sheria ya Ushindani, Na. 8/ 2003. Pia tahadhari inatolewa kwa wahusika wote kuwa makini na vitendo vya kugoma kuuza bidhaa au hudumu ili kuepuka hatua kali za kisheria kuchukuliwa dhidi yao.


NOTISI HII IMETOLEWA NA TUME YA USHINDANI

TAREHE 19 Septemba, 2014




FREDERICK RINGO
MKURUGENZI MKUU
TUME YA USHINDANI

No comments:

Post a Comment