Sunday 14 September 2014

FCC Yakamata SImu Bandia za Sh Mil 72.25



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

FCC Yakamata Simu Bandia za Sh. 72.25m/-

Dar es Salaam, Septemba 13, 2014. Tume ya Ushindani imeendesha zoezi la ukaguzi wa kushtukiza katika eneo la Kariakoo na kukamata simu bandia za mkononi aina ya Samsung na Blackberry.

Zoezi hilo lililofanyika Septemba 11, 2014 liliwezesha kukamatwa kwa simu bandia 289 zenye jumla ya thamani ya Sh. 72,250,000.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa thamani iliyotajwa ya bei ya soko ya simu hizo bandia ni robo tu ya thamani ya simu halisi, lakini simu hizo bandia zilizokamatwa baadhi zilikutwa zimefungashwa kwenye maboksi ya simu halisi.

Wamiliki wa Maduka yaliyokaguliwa na simu bandia kupatikana yanamilikiwa na Hamadi Bakari Hamadi (simu 27), Hamadi Juma Musa (simu 62 na maboksi matupu 47), Fatuma Gharib Mohammed (simu 72 na betri 5), Jarade Zahor Mohammed (simu 47), Selemani Juman Selemani (simu 35) na Bakari J. Khatib (simu 44 na simu moja isiyo na nembo iliyokuwa ikifanana na  simu za Samsung pamoja na simu moja bandia ya Blackberry).

Wafanyabiashara husika wote walipatiwa hati za kukamatiwa bidhaa zao. Aidha wahusika walitoa maelezo katika kituo cha polisi cha Msimbazi kuhusiana na na kukamatwa na bidhaa hizo ili hatua zaidi za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Wafanyabiashara husika wamekwishaagizwa hatua za kuchukua kwa mujibu wa Sheria ya Alama za Bidhaa, inayokataza biashara ya bidhaa bandia. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, wafanyabishara wanaokamatwa na bidhaa bandia hutakiwa kulipa faini stahiki pamoja na gharama za uteketezaji wa shehena za bidhaa zilizokamatwa, kulingana na tathmini inayofanyika kuhusiana na bidhaa hiyo.

Zoezi hilo la ukaguzi wa kushitukiza lilitokana na maombi ya Wawakilishi wa Hataza na Alama za Biashara za Samsung, Kampuni ya “Anti Illicit Trade”, yenye makao yake jijini Nairobi, Kenya.

Ukaguzi wa kushitukiza na ukamataji wa bidhaa bandia ni zoezi endelevu. Kwa mantiki hiyo, Tume ya Ushindani inawaasa wafanyabishara wote kujiepusha na kuagiza, kusarifisha, kuchukua bidhaa hizo toka wakala feki na kujishughulisha na bishara ya bidhaa bandia kwa kuwa ni kosa la jinai linaloambatana adhabu kali za faini na kifungo.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani ni Mkaguzi Mkuu wa Sheria ya Alama za Bidhaa mwenye jukumu la kuongoza mapambano dhidi ya bidhaa bandia katika soko la Tanzania bara. Sheria inampa mamlaka Mkaguzi Mkuu kufanya ukaguzi wa mizigo na bidhaa katika maingilio yote ya bidhaa pamoja na maduka, maghala na maeneo yanayomilikiwa na watu binafsi yanayohofiwa kuficha au kuhodhi bidhaa bandia.
Sheria pia inampa Mkaguzi Mkuu mamlaka ya kukamata bidhaa zinazoshukiwa kuwa bandia pamoja na kutoa adhabu za kiutawala ambazo ni pamoja na adhabu za kutoza faini na gharama za uteketezaji wa bidhaa zilizokamatwa na kuthibitishwa kuwa ni bandia.

Imetolewa leo Septemba 13, 2014 na



Frederick Ringo
MKAGUZI MKUU, SHERIA YA ALAMA ZA BIDHAA

No comments:

Post a Comment