Tuesday 5 December 2017

FCC Yaadhimisha Siku ya Ushindani Desemba 5, 2017

Dar es Salaam, Desemba 6, 2017. Tume ya Ushindani nchini Tanzania imeadhimisha Siku ya Ushindani Duniani kwa kutoa mafunzo kwa wadau wa vyombo vya udhibiti na wawakilishi wa vyama vya wafanyabiashara.

Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 5 Desemba, 2017 katika ukumbi wa GEPF, eneo la Victoria na Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Mhandisi Stella Manyanya (MB), alikuwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo.

Akifungua Rasmi maadhimisho hayo, Mhe. Naibu Waziri Manyanya aliwataka Wafanyabiashara kuepuka kuigeuza Tanzania jalala la bidhaa bandia. Aidha aliwaonya watendaji wa Serikali kuepukana na vishawishi vya rushwa katika kukagua bidhaa sokoni na katika maingilio ya bidhaa nchini.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani, Dk. John Kedi Mduma alimweleza Naibu Waziri kuwa maadhimisho hayo yametokana na Makubaliano ya Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa yaliyofanyika  tarehe 5 Desemba, 1980 ya kukubaliana kuhusu kanuni za kudhibiti vitendo vinavyodumaza ushindani duniani. Alibainisha kuwa nchi wanachama zinaadhimisha siku hii kuendelea kuwakumbusha watendaji katika mfumo wa biashara ulimwenguni kuzingatia misingi na kanuni za ushindani.

Mafunzo hayo yalihudhuriwa na watendaji kutoka Wakala wa Mbolea, Shirika la Viwango (TBS), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (EWURA), Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Chama cha Wenye Viwanda, Biashara na Kilimo (TCCIA), Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Anga (TCAA), Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na wadau wengine.

Wadau hao pia waliweza kuelezea uzoefu wao katika kushajiisha ushindani katika soko katika utekelezaji wa shughuli zao. 

No comments:

Post a Comment